Thursday, February 12, 2015

WAKANDARASI RUVUMA WALIA NA TANROAD



Na Julius Konala,
Songea.

BAADHI ya Wakandarasi mkoani Ruvuma, wameilalamikia serikali kupitia Wakala wa barabara Tanzania (TANROAD) mkoani humo, kutokana na ucheleweshaji wa malipo yao ya kazi walizofanya, katika mwaka wa fedha wa 2014/2015 hali ambayo sasa, inawafanya waishi katika mazingira magumu.

Wakizungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti mjini hapa, wakandarasi hao ambao hawakutaka majina yao yatajwe walisema kuwa hali zao hivi sasa ni mbaya, kutokana na kudaiwa na taasisi za kibenki ambako walikuwa wamekopa fedha, kwa ajili ya kuendeshea shughuli za miradi waliyopewa na TANROAD.

Walidai kuwa baadhi yao mali ambazo waliweka kama dhamana, taasisi hizo za fedha wameanza kutaifisha na kutokana na kuchelewesha kurejesha mikopo waliyokopa kwa wakati, hali ambayo inawafanya kuwaingiza kwenye umasikini mkubwa na kuvunja mahusiano baina yao na hata wamiliki wa maduka, ambako walikopa vifaa vya ujenzi na kukodi mitambo kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli husika.


Walifafanua kuwa kucheleweshwa kwa malipo hayo ya fedha, kupitia akaunti ya miradi ya maendeleo imewafanya washindwe kuwalipa vibarua, kulipia fedha za kukodishia mitambo pamoja na gharama za uendeshaji, hivyo wamedai kwamba kutokana na mitaji yao kuwa midogo wanashindwa kufanya kazi.

Akizungumza kwa niaba ya wakandarasi wenzake, Ally Mohamed alisema kutokana na waajiri wao kushindwa  kuwalipa mishahara yao, kwa muda mrefu wamekuwa wakikumbana na matatizo mbalimbali, yakiwemo kushindwa kumudu gharama za matibabu, kuwapeleka watoto wao shule, kulipia kodi ya nyumba pamoja na kununua mbolea kwa ajili ya kuendeleza shughuli za kilimo.

“Hali hii imetufanya tuishi katika mazingira magumu sana, kwani tunashindwa hata kuwa na fedha kwa ajili ya kununua chakula pamoja na kulipa kodi ya nyumba, jambo hili linatufanya hata kutokuwepo na maelewano mazuri baina yetu na wamiliki wa nyumba”, alisema Mohamed.

Hata hivyo alipotafutwa Meneja wa TANROAD mkoani Ruvuma, Abraham Kisimbo kwa ajili ya kutolea ufafanuzi kuhusiana na malalamiko hayo, hakuweza kupatikana na hata simu yake ilikuwa ikiita kwa muda mrefu bila kupokelewa.

No comments: