Thursday, February 12, 2015

VYAMA VYA WAFANYAKAZI NCHINI FUNGUKENI KUSAIDIA WANACHAMA WENU



Na Mwandishi wetu,

NIMECHUKUA jukumu la kuvishauri vyama vya wafanyakazi pamoja na shirikisho la wafanyakazi hapa nchini, kutokana na hali halisi ya utatanishi kati ya waajiri na wafanyakazi katika mahusiano yao. Mahusiano hasi kati ya mwajiri na mwajiriwa yamekuwa nikawaida katika mazingira ya kazi hapa nchini.

Binafsi naamini vyama vya wafanyakazi ni kiungo kati ya waajiri na wafanyakazi hivyo kuwa daraja katika kushughulikia kero, changamoto au matatizo mbalimbali kati ya mwajiri na mfanyakazi, pia hushughulikia kutoa msaada wa kisheria kwa inapobidi.

Licha ya hapa kwetu Tanzania, kuwa na vyama vya wafanyakazi pamoja na juhudi mbalimbali za vyama hivyo bado kumekuwa na changamoto nyingi zinazowakabili wafanyakazi.

Hivyo upo umuhimu wa vyama hivyo kushirikiana na taasisi binafsi kutoa msaada wa kisheria pamoja na elimu kwa wafanyakazi, ili kuondoa hali ya manyanyaso, ukiritimba na urasimu unaofanywa na waajiri kazini.


Leo hii tunaelekea Mei mosi, maadhimisho ya wafanyakazi wote nchini, je ni lipi la kujivunia sisi kama wafanyakazi? je kama wafanyakazi tumeweza kupata mafanikio kutokana na changamoto zile zilizotukumba kabla ya Mei mosi ya 2014? je ipi ni taswira ya vyama au mashirikisho ya vyama vya wafanyakazi? je wafanyakazi wana taswira chanya au hasi dhidi ya vyama au shirikisho la wafanyakazi? je kwa nini wanamtazamo chanya au hasi dhidi ya vyama au shirikisho la wafanyakazi?

Najua changamoto kubwa itakuwa ni wafanyakazi wengi kutokuwa tayari kujiunga na vyama vya wafanyakazi, kuchangia ada zao au kuwa tayari kujiunga na vyama vya wafanyakazi kwa kujaza fomu namba TF6 kwa ajili ya kuhudhuria nakukubaliana na vyama vya wafanyakazi? je kwa muda huu wa mwaka mmoja toka tuadhimishe sikukuu ya wafanyakazi tumepiga hatua au tumerudi nyuma?

Je vyama vimetoa elimu kwa wanachama au wafanyakazi wao, juu ya wajibu na stahiki zao muhimu? je ni kwa kiasi gani vyama vimeweza kutoa msaada wa kisheria kwa wanachama wao? je ni kwa namna gani vyama vimekuwa na ushawishi ambao umesaidia wanachama wao kujiunga kwa hiari, ili kuweza kupanua wigo wa kuwasaidia wafanyakazi wengi zaidi?

Je ni kwa namna gani vyama vya wafanyakazi, vimeweza kutatua migogoro ya kazi bila kuathiri shughuli za mwajiri? je ni kwa namna gani vyama hivyo vimeweza kuwadhibiti waajiri wanaoenda kinyume na taratibu au kanuni za mahusiano kazini kati ya mwajiri na mfanyakazi?

Haya ni maswali yangu tu machache lakini, nitatolea mifano kadha wa kadha inayoweza ikasaidia kuonyesha ni kitu gani kinatakiwa kifanyike, ili kunusuru hali ya wafanyakazi hasa wanaoajiriwa kiholela bila mikataba wala mfumo rasmi wa malipo, hii inatokana na uzoefu wangu nilioweza kuupata kwa muda mfupi baada tu, ya kujihusisha kupigania haki stahiki za wafanyakazi.

Nimekuwa nikifuatilia ajira za walinzi binafsi, katika sekta binafsi na zile za umma mfano masokoni, maduka, shule na hata ofisi za umma, pia ajira za upishi katika shule za msingi na sekondari naamini hizi zote ni ajira ambazo zinatakiwa kuheshimiwa, na wapo kwa ajili ya kuwasaidia waajiri ili waweze kutimiza adhma yako kutokana na malengo yao binafsi au ya taasisi husika.

Pia zipo ajira zinazotolewa kwenye sehemu za starehe maarufu kama bar, grosary, mahotelini nakadhalika nao kwa upande wao kunachangamoto nyingi hasa dhidi ya ukatili wa wanawake, kudhalilishwa na kunyanyaswa nako huku tunasikia vipo vyama vinavyowatetea. Pia hata wale wafanyakazi wanaofanya kazi majumbani (House boy na House girl) nao wanachangamoto nyingi je nani anawajali?

Haya yote yanatokea ikiwa tuna serikali inayotoa miongozo kila mwaka, chini ya Wizara ya kazi ajira na vijana juu ya viwango vya mishahara kwa sekta binafsi na umma, lakini mwisho wake hayupo mtu au taasisi binafsi inayowalipa walinzi, wapishi, wafanyakazi kwenye sehemu za starehe, mahouse girl na house boy?

Nani awasaidie wafanyakazi hawa wajue stahiki zao, au nani awasaidie kutatua migogoro kati yao na waajiri wao ikiwa tu kila wanapodai stahiki zao wanaishia kubambikizwa kesi, kupigwa na hata wengine kufukuzwa kazi lakini vyama vya wafanyakazi vimebakia kuwa na ofisi mijini tu.

Kundi hili utakuta linapewa ajira bila mikataba, hivyo hata inapofikia muda utakuta kuna migogoro, wakati huo wafanyakazi hawa hawana pa kusimamia na chakuumiza zaidi hawana elimu yoyote ile ya haki na wajibu wa mfanyakazi, elimu dhidi ya viwango vya ujira kwa kazi zao, je nani awasaidie?

Ni imani yangu mfanyakazi akiwa ametimiza wajibu wake inatakiwa apewe stahiki sahihi hivyo, nashauri ni vyema waajiri wakaliona hilo na pia vyama vya wafanyakazi vione haja ya kuwasaidia wafanyakazi, ambao ndio wanachama wao kwa kuwapatia taarifa sahihi ikiwa pamoja na haki stahiki, nyaraka maalum za malipo na pia ikiwa pamoja na msaada wa kisheria pale inapobidi.

Ushauri wangu, itakuwa ni kichekesho kwa vyama vya wafanyakazi kuishia kuadhimisha maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani (Mei Mosi) huku wafanyakazi wake wakiwa wanaishi maisha duni, yenye manyanyaso, dhuluma na chuki. Pia itakuwa ni kichekesho kwa vyama vya wafanyakazi nchini, vikiwa na taswira hasi dhidi ya wanachama wao maana utakuwa ni mwanya kwa waajiri kuendelea kuwakandamiza wafanyakazi.

No comments: