Wednesday, February 18, 2015

MTOTO SOPHIA ABDUL ANAOMBA MSAADA WA MATIBABU KWA WASAMARIA WEMA

Mtoto Sophia Abdul, ambaye ana tatizo la jicho.

Na Amon Mtega,
Songea.

MTOTO Sophia Abdul (14) ambaye ana matatizo ya ugonjwa ambao bado haufahamiki jina lake, umejitokeza katika jicho lake la upande wa kulia ambalo limevimba na kujitokeza nje, anaomba msaada wa matibabu ili aweze kunusuru afya yake.

Sophia anasoma shule ya msingi Lilahi darasa la tano, iliyopo kata ya Mhukulu wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, amekumbwa na ugonjwa huo ambao unamletea maumivu makali na kushindwa kwenda shule, kuhudhuruia masomo yake.

Akizungumza na waandishi wa habari, katika ofisi za elimu wilayani humo mama wa mtoto huyo ambaye alijitambulisha kwa jina la, Joyce Nyoni alisema mwanae alianza kupatwa na ugonjwa huo tangu mwezi Aprili mwaka jana, ambapo jicho hilo lilianza  kuwasha na kujitokeza uvimbe, ambao kwa sasa umesababisha kushindwa hata kuona.

Mama huyo alisema anaomba wasamaria wema popote pale walipo, wamsadie ili mwanae aweze kutibiwa na hatimaye kupona, ili aweze kuendelea na masomo yake.


Aidha alifafanua kuwa baada ya kuona hali ya mwanae inazidi kuwa mbaya, alimpeleka katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Ruvuma na kukutana na madaktari ambao walimwambia kuwa ugonjwa huo, hawataweza kuutibu na kutambua ni waina gani na nini hasa kinachomsumbua Sophia, badala yake walimtaka atafute fedha ampeleke katika hospitali ya rufaa ya Muhimbili.

Joyce baada ya kupata maelekezo ya madaktari, aliamua kupita kuomba msaada kwa wasamaria wema ili kunusuru maisha ya mwanae kwa kuwa yeye mwenyewe hivi sasa hana uwezo wa kifedha na kwamba baba wa mtoto huyo, Abdul Rashid alimtelekeza toka akiwa na umri wa mwaka mmoja.

Alisema kufuatia hali hiyo mwanae hajahudhuria masomo toka walipofungua shule mapema Januari mwaka huu, jambo ambalo linaweza kumrudisha nyuma katika maendeleo yake kimasomo na haki ya kupata elimu.

Kadhalika aliongeza kuwa wakati akiwa katika hospitali hiyo ya mkoa, aliambiwa na madaktari hao kuwa, pindi atakapopata fedha za matibabu watamwandikia kibali cha kumruhusu kwenda kupata matibabu huko Muhimbili.

Hata hivyo, mama wa mtoto huyo anawaomba wasamaria wema kutoa mchango wao wa hali na mali ili aweze kufanikiwa kumpeleka mwanae kwenye matibabu, kiwango cha fedha kinachohitajika hadi sasa hakifahamu kutokana na ugonjwa wenyewe kutojulikana ni wa aina gani, ambapo kwa atakayeguswa na tatizo hilo la mtoto Sophia, watoe michango yao kwa simu namba; 0683115075 ambayo ni ya mama ya mtoto huyo.

No comments: