Saturday, February 14, 2015

MTOTO WILAYANI TUNDURU AZALIWA NA ULEMAVU UTUMBO UKIWA NJE

Na Steven Augustino,

Tunduru.

MTOTO mchanga mwenye jinsia ya kike wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, amezaliwa katika Hospitali ya wilaya hiyo, huku akiwa na ulemavu ambapo utumbo wake umejitokeza kwa nje.

Taarifa za tukio hilo ambalo limesisimua baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo, zinaeleza kuwa mtoto huyo ambaye amezaliwa na Bi. Theresia George (25) lilitokea usiku wa kuamkia Februari 2 mwaka huu.

Wauguzi waliokuwa zamu katika hospitali hiyo, walionesha kushitushwa na tukio hilo na kuwafanya watoe taarifa za kuomba msaada kwa madaktari wenzao, ili waweze kupatiwa ufumbuzi zaidi juu ya tukio hilo.

Akizungumzia tukio hilo, mama wa mtoto huyo Theresia George alisema, yeye asili yake ametokea mkoani Mbeya na sasa anaishi katika kijiji cha Mtina wilayani Tunduru.


Maafisa tabibu ambao waloshudia tukio hilo, akiwemo mganga mkuu wa wilaya hiyo Dokta Alex Kazula alisema kuzaliwa kwa mtoto huyo akiwa na ulemavu huo wa viungo utumbo kutoka nje, ni miongoni mwa matukio ya kawaida ambayo yamekuwa yakijitokeza hapa duniani.

Dokta Kazula alifafanua kuwa, baada ya tukio hilo yeye kwa kushirikiana na madaktari wenzake wa hospitalini hapo, walifanya uchunguzi pamoja na kufanya mawasiliano na madaktari bingwa ikiwa ni lengo na juhudi za kuokoa maisha ya mtoto huyo.

Alisema wakati hayo yanafanyika, mtoto huyo alipelekwa hospitali ya misheni Mbesa wilayani humo, ambayo ina dakatari bingwa wa magonjwa ya upasuaji ambako baadaye mtoto alifariki dunia akiwa ameishi kwa muda wa siku mbili.

Kwa mujibu wa Dokta Kazula, alisema alizaliwa akiwa na upungufu ambao kwa lugha ya kitaalamu unaitwa (Congnital malfamation) ambao hutokea wakati wa uumbaji wa viungo vya mwili, vinapokuwa vikitengenezwa au kuundwa tumboni mwa mama.

“Ukosefu wa baadhi ya viungo vya mwili, hujitokeza wakati vinapoundwa mtoto akiwa tumboni (Organ genesis) ugonjwa huu, Ophalocele hujitokeza sehemu yoyote ya mwili”, alisema.

Pamoja na mambo mengine alieleza kuwa, ugonjwa huo huweza kuathiri viungo mbalimbali vya mwili wa mtoto, na kuleta madhara makubwa katika moyo, tumbo na kwenye ubongo.

Dokta Kazula aliendelea kusema kuwa miongoni mwa vyanzo vya matukio ya mtoto kupata ugonjwa wa namna hiyo, husababishwa na mama mjamzito kunywa pombe kupita kiasi, uvutaji wa sigara pamoja na matumizi ya dawa bila kupata ushauri wa maafisa tabibu, hasa katika kipindi cha miezi mitatu ya kwanza ya ujauzito wake.

Hata hivyo mganga huyo aliwataka watu kuacha tabia ya kuwanyanyapaa wanawake ambao wamekuwa wakijifungua watoto wenye ulemavu,ambao kwa namna moja au nyingi huwa na mapungufu ya viungo vya mwili.

No comments: