Tuesday, February 24, 2015

MASHINE BVR BALAA ZAKATAA KUTAMBUA WENYE VIDOLE SUGU



Na Thobias Mwanakatwe,

ZOEZI la uandikishaji wapigakura katika Daftari la Kudumu la Wapigakura limeanza katika Mkoa wa Njombe, huku likikabiliwa na changamoto nyingi, ikiwamo mashine za Biometric Voter Registration (BVR) kushindwa kutambua watu wenye vidole vyenye michilizi.

Kujitokeza kwa kasoro hizo kumekuja siku tatu tangu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, alipoeleza kuwa amenasa nyaraka zinazoonyesha Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), ilishauriwa na mtaalam kutoka Marekani kwamba Tanzania haijawa tayari kwa teknolojia ya BVR.

Mwenyekiti wa Nec, Jaji mstaafu Damian Lubuva, akizungumza na NIPASHE alisema zoezi la uandikishaji limeanza katika mkoa wa Njombe na kwamba viongozi wa tume hiyo wapo kwa ajili ya kusimamia kuhakikisha kunakuwa na mafanikio.

Jaji Lubuva alipoulizwa kama tume imeanza na BVR ngapi, alisema suala hilo hawezi kulijibu. Hivi karibuni kuriripotiwa kuwa Nec imepata BVR 250 tu kati ya 8,000 zinazotakiwa.


“Nipo Njombe ndiyo tumeanza zoezi la kuandikisha, suala  la kwamba tumeanza na BVR ngapi sina jibu, kwanza nipo kwenye kikao,”alisema Lubuva na kukata simu. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Nec, Julius Malaba, alisema uzinduzi rasmi wa uandikishaji katika mkoa wa Njombe utafanyika leo.

Malaba alisema dosari ambazo zimeelezwa kujitokeza watazitolea ufafanuzi na kuzitafutia ufumbuzi.

Kasoro nyingine zilizojitokeza ni uchache wa vifaa,watoa huduma waliopewa jukumu hilo kushindwa kutumia mashine na kulazimika kutumia muda mwingi kumwandikisha mtu mmoja hali inayotia wasiwasi kwamba huenda siku saba zilizopagwa kufanyika kwa kila mkoa kushindwa kufikia malengo.

Uandikishaji huo ulianza jana katika Halmashauri ya Mji wa Makambako na mamia ya wananchi wakijitokeza katika vituo vya kujiandikisha lakini baadhi yao walijikuta wakikwama kutokana na mashine za BVR kushindwa kuwatambua kutokana na aina ya vidole walivyokuwa navyo.

Mmoja wa wakazi wa mji wa Makambako, Orahp Mhema, alisema katika vituo walivyoenda kujiandikisha wameshidwa kuingiza maelezo yao ya kibaolojia kwa sababu mashine zinazotumika kushindwa kutambua vidole vyao kutokana na mikono yao kuwa na michilizi inayotokana na shughuli za kila siku, ikiwamo kilimo.

Alisema katika zoezi hilo kuna wasiwasi wa watu wengi kushindwa kuandikishwa kutokana na muda  wa siku saba uliopangwa kuwa mdogo hasa ikizingatiwa kuwa waandikishaji wanatumia muda mrefu kuhudumia mtu mmoja. Mhema alisema  mbali na changamoto ya mashine kufanyakazi taratibu pia katika zoezi hilo kumejitokeza tatizo la watoa huduma kushindwa kuzitumia mashine kikamilifu kutokana na elimu ya kutumia mashine hizo kutowafukia mapema.

"Katika zoezi hili wananchi wamehamasika kujiandikisha lakini wanakwamishwa na mashine hizo kufanya taratibu na baadhi yao kushindwa kuzitumia kikamilifu na nimeshuhudia mmoja akishindwa kubonyeza baadhi ya batani katika mashIne," alisema Mhema.

Aliongeza : "Watu wengine wamechukuliwa taarifa nyingine kwa kuwa vidole vyao vimeshindwa kutambuliwa na mashine hizo kwa kuwa inamikwaruzo mbalimbali inayotokana na ufanyaji wa kazi za kila siku," aliongeza.

Watu walioshindwa kutambuliwa na mashine wengi wao wamejaribu kurudia zaidi ya mara moja, baadhi yao mashine zimekubali na wengine zimeshindwa kabisa kuwatambua.

Naye  Sifaely Msigala alisema licha ya wananchi kujitokeza kwa wingi, lakini wameshindwa kufanikiwa na kukwama kuendelea na shughuli zao kutokana na kushinda mda mrefu katika  vituo vya uandikishaji wa daftari hilo.

Alisema kama kasi ya mashine hizo itaendelea kama ilivyo kuna uwezekano mkubwa zoezi hilo kushindwa kufanikiwa kwani wananchi wengine watakuwa wameshindwa kuandikishwa. 

Februari 12, mwaka huu, Nec ilikutana na vyama vya siasa 21 , ambao ni wadau muhimu katika suala zima la uchaguzi na agenda kuu ilikuwa kuzungumzia mfumo wa BVR. Nec ilitoa taarifa ya jinsi zoezi la majaribio katika baadhi ya kata za majimbo ya Kawe, Kilombero na Mlele lilivyoendeshwa na changamoto zilizojitokeza na matarajio ya kuendesha katika mikoa ya Lindi, Ruvuma na Njombe, lakini kutokana na uhaba wa vifaa wataanza na  wa Njombe.

Katika mkutano huo,  Jaji Lubuva alisema vifaa vilivyopo ni 250 na kwamba 7,750 vinasubiriwa ili kufanikisha  zoezi hilo kufanyika nchi nzima.

Kuhusu fedha, alisema zimetolewa asilimia 50 na wana imani kubwa serikali itatoa kiasi kilichobaki kwa wakati.

Kwa upande wa ratiba, alisema itawekwa wazi baada ya kumaliza zoezi la Njombe na vifaa vinavyosubiriwa kuwasili.

Katika moja ya maelezo ya Tume huko nyuma ni kuwa wangetoa elimu na taarifa mbalimbali kupitia tovuti yao, lakini hadi sasa ina taarifa za mwaka 2007 na majibu ya Mwenyekiti ni kuwa kwa sasa wanaifanyia kazi.  

CHADEMA WAZUNGUMZA

Nacho Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kisema  kimebaini kasoro mbalimbali zilizojitokeza kwenye mji wa Makambako.

Dosari hizo zimebainika baada ya Naibu Katibu  wa Chadema Bara, John Mnyika na viongozi wengine wa chama hicho kufanya ziara ya kutembelea kwenye vituo vya uandikishaji

Mnyika alitaja dosari walizozibaini kuwa ni mashine za BVR kutofanya kazi kwa zaidi ya saa sita na kugoma kuchukua alama za vidole sugu ambazo zimetokana na kazi ngumu.

Alivitaja vituo ambavyo mashine zilizogoma kufanya kazi kuwa ni  cha Malombwe na Liamkena ambako uandikishaji ulikuwa ni wa kusuasua na kusababisha watu watano kuandikishwa kwa saa nne. 

Februari 12, mwaka huu, Nec ilikutana na vyama vya siasa 21 , ambao ni wadau muhimu katika suala zima la uchaguzi na agenda kuu ilikuwa kuzungumzia mfumo wa BVR. Nec ilitoa taarifa ya jinsi zoezi la majaribio katika baadhi ya kata za majimbo ya Kawe, Kilombero na Mlele lilivyoendeshwa na changamoto zilizojitokeza na matarajio ya kuendesha katika mikoa ya Lindi, Ruvuma na Njombe, lakini kutokana na uhaba wa vifaa wataanza na  wa Njombe.

Katika mkutano huo,  Jaji Lubuva alisema vifaa vilivyopo ni 250 na kwamba 7,750 vinasubiriwa ili kufanikisha  zoezi hilo kufanyika nchi nzima.

Kuhusu fedha, alisema zimetolewa asilimia 50 na wana imani kubwa serikali itatoa kiasi kilichobaki kwa wakati.

Kwa upande wa ratiba, alisema itawekwa wazi baada ya kumaliza zoezi la Njombe na vifaa vinavyosubiriwa kuwasili.

Katika moja ya maelezo ya Tume huko nyuma ni kuwa wangetoa elimu na taarifa mbalimbali kupitia tovuti yao, lakini hadi sasa ina taarifa za mwaka 2007 na majibu ya Mwenyekiti ni kuwa kwa sasa wanaifanyia kazi.  Chanzo Nipashe.

No comments: