Tuesday, February 17, 2015

OFISA UTUMISHI MBINGA ALALAMIKIWA NA WATUMISHI WAKE

Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

EMMANUEL Kapinga, ambaye ni Ofisa utumishi wa Halmashauri ya wilaya Mbinga mkoani Ruvuma, analalamikiwa na baadhi ya watumishi wenzake wa kada mbalimbali katika halmashauri hiyo wakidai kwamba, amekuwa akiwatolea lugha mbaya zenye kukatisha tamaa na kutowasikiliza pale wanapopeleka hoja au matatizo yao ya msingi, ili yaweze kufanyiwa kazi na kupatiwa ufumbuzi. 

Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi kwa muda mrefu sasa, umebaini hata taratibu za maboresho kwa mfanyakazi, kama vile kupandishwa cheo au kwenda masomoni, imekuwa ni tatizo kwa Ofisa utumishi huyo kuyapitisha kwa wakati, jambo ambalo ndio maana analalamikiwa.

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu vya habari, vilifafanua kwa nyakati tofauti kuwa mnamo mwezi Julai mwaka jana serikali iliweka utaratibu kwamba, watumishi wote wenye daraja la TGS A wanafuta daraja hilo, na badala yake wapandishwe vyeo kufikia TGS B lakini katika halmashauri ya wilaya hiyo, Kapinga analalamikiwa akidaiwa kutolifanyia kazi jambo hilo ipasavyo kwa kuwapandisha vyeo baadhi ya watumishi wenzake, na kufanya kuwepo na malalamiko yasiyokuwa na msingi.

“Baadhi ya watumishi mpaka sasa hatujapandishwa vyeo wala mishahara, licha ya serikali kuagiza jambo hili lifanyiwe kazi haraka, tokea mwezi Julai mwaka jana”, walisema.

Aidha Mkuu huyo wa idara ya utumishi wilayani humo, ananyoshewa kidole kuwa mtumishi ambaye anaomba kuingizwa kwenye mpango kwa ajili ya kwenda masomoni, kwa lengo la kujiendeleza cheo alichonacho napo imekuwa ni tatizo kufanyiwa utekelezaji husika na kuishia kupewa lugha zisizoridhisha.


Vilevile Kapinga, amekuwa akishutumiwa kufanya mchezo mchafu wa kunyofoa nyaraka muhimu ya mtumishi ambaye amekubaliwa na kuingizwa kwenye mpango wa kusomeshwa na serikali, na kulazimisha asaini mkataba binafsi wa kwenda kujisomesha mtumishi mwenyewe na sio serikali.

Habari zinaeleza kuwa, kitendo hicho kinachofanywa na mtumishi huyo ambaye serikali ilimuamini na kumpatia idara nyeti kama hiyo, kwa ajili ya kuweza kufafanua sera za utumishi wa umma kwa watumishi wenzake wa kada mbalimbali ndani ya halmashauri, ni cha ubabe ambao haupaswi kuvumiliwa hivyo achukuliwe hatua za kinidhamu ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo. 

Walidai kuwa hata kwa wale ambao wanadai fedha zao za uhamisho tokea mwaka 2011 mpaka sasa, hawajalipwa madai yao na kubaki wanazungushwa bila kupewa majibu yanayojitosheleza.

Kadhalika Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani Mbinga, taarifa za uhakika zilizotufikia mezani kwetu imepelekewa malalamiko kama hayo na kutoa majibu yanayochelea kwamba, itayafanyia kazi huku ikijua fika halmashauri hiyo, kumekuwa na uozo wa mambo mengi ambayo inabidi yafanyiwe kazi kwa haraka na kuweza kuleta haki sawa katika jamii.

Ditram Mhoma ambaye ni Kamanda wa TAKUKURU wa wilaya hiyo, amekuwa akitoa majibu kwa waandishi wa habari mara kwa mara kwamba, ofisi yake inafanyia kazi lalamiko lolote la msingi linaloletwa na mwananchi yeyote na uchunguzi unapokamilika hatua za kisheria huchukuliwa dhidi ya mtuhumiwa.

Ofisa utumishi wa wilaya ya Mbinga, Kapinga alipozungumza na mwandishi wetu juu ya tuhuma hizo ofisini kwake alikataa kuzungumzia malalamiko hayo na kumwambia; “nenda kwanza kwa Mkurugenzi ukapate kibali cha kuzungumza nami akikuruhusu nipo tayari kutoa ufafanuzi wa jambo lolote”.

Mwandishi wetu alipochukua hatua ya kwenda kumwona Mkurugenzi mtendaji wa wilaya hiyo, ambaye alikuwa akikaimu nafasi hiyo, Oscar Yapesa alitoa ushirikiano na kuruhusu kwenda kuzungumza naye ambapo Kapinga alipotakiwa kutoa ufafanuzi juu ya malalamiko hayo, alikana na kusema kuwa hakuna ukweli juu ya mambo hayo.

No comments: