Thursday, December 21, 2017

HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA YAINGIA MKATABA MKOPO WA VIFAA VYA BILIONI 1.2 KUKAMILISHA UJENZI MIRADI YA WANANCHI VIJIJINI

Afisa mipango wa wilaya ya Mbinga, Onesmo Mapunda.


Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

HALMASHAURI ya Wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imeingia mkataba wa kukopa vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.2 na Kampuni ya Kisarawe Cement Company Limited na M.M Intergrated Mills Company Limited, ili kuweza kukamilisha ujenzi wa miradi ya maendeleo ya wananchi vijijini.

Aidha imeelezwa kuwa makampuni hayo yapo jijini Dar es Salaam na kwamba mpaka sasa vifaa walivyoanza kuchukua baada ya kuingia mkataba huo ni vya shilingi milioni 462 na kwamba tayari vifaa vya shilingi milioni 150 vimesambazwa katika miradi ya wananchi wilayani humo.

Afisa Mipango wa halmashauri ya wilaya hiyo, Onesmo Mapunda alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake, juu ya jukumu la halmashauri hiyo kutoa huduma endelevu za kijamii na kiuchumi kwa wananchi wake.


Mapunda alifafanua kuwa lengo kubwa la kufanya hivyo ni kuweza kupunguza kero zilizodumu kwa muda mrefu ili wananchi waweze kupata huduma kwa ukaribu ikiwemo za afya na elimu ili wanafunzi nao waweze kusoma katika mazingira mazuri.

Alisema kuwa katika wilaya ya Mbinga, kuna miradi 600 ambayo inahitaji kukamilishwa ujenzi wake na kwamba licha ya wilaya kuwa na vijiji 121 lakini zahanati ambazo zimekamilika ujenzi huo ni 54 tu.

Kufuatia hali hiyo uongozi wa halmashauri kwa kushirikiana na Madiwani wake waliona ni vyema waingie mkataba huo wa kukopa vifaa ili kuweza kufikia malengo husika ya kukamilisha miradi yote viporo iliyopo wilayani hapa.

Kadhalika alibainisha kuwa miradi ambayo mpaka sasa imepelekewa vifaa hivyo vijijini kwa wananchi ni ya ujenzi wa zahanati, ukamilishaji wa vyumba vya maabara, vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari, nyumba za watumishi pamoja na mabweni ya kulala wanafunzi.

Afisa mipango huyo aliongeza kuwa miradi 162 iliyopo katika kata 29 za wilaya ya Mbinga, mpaka sasa tayari imekwisha pelekewa vifaa vya ujenzi ikiwemo bati, saruji, misumari, nondo na yapo baadhi ya maeneo tokea vifaa hivyo vigawiwe wananchi wameweza kushiriki kikamilifu katika ujenzi huo.

Pia alibainisha kuwa wanakopa vifaa hivyo vya ujenzi katika makampuni hayo na hapo baadaye wakipata fedha kutokana na mapato yao ya ndani watakuwa wakilipa fedha kwa awamu kulingana na makubaliano husika yaliyopo kwenye mkataba wao.

No comments: