Monday, December 18, 2017

VIJANA WATAKIWA KUACHA TABIA YA KUKAA VIJIWENI


Na Dustan Ndunguru,
Mbinga.

MKURUGENZI wa vijana jimbo katoliki la Mbinga mkoani Ruvuma, Padri Donatus Komba amewataka vijana kuacha tabia ya kukaa vijiweni bila kufanya kazi, badala yake wajiunge pamoja na kuanzisha vikundi vya ujasiriamali ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Padri Komba ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Kindimba alisema hayo wakati alipokuwa akihubiri katika kanisa hilo hivi karibuni na kusema kuwa, kitendo kinachofanywa na vijana kukaa na kucheza kamali vijiweni katika kijiji cha Kindimba kinapaswa kukemewa kwa nguvu zote ili kuwanusuru wasiharibikiwe katika maisha yao.

Alisema kuwa vijana ni kundi linalotegemewa katika kuendeleza taifa lolote lile kwa mustakabali wa maendeleo husika hivyo wazazi na walezi wanakila sababu ya kuhakikisha wanatoa maelekezo yaliyosahihi kwa watoto wao ili wasijiingize kwenye vitendo viovu.


Padri huyo alifafanua kuwa mchezo wa kamali ambao umeshamiri katika kijiji hicho umesababisha kushamiri kwa vitendo vya wizi ambavyo vimekuwa vikisababisha wananchi kuibiwa katika maeneo mbalimbali kijijini humo na kwamba viongozi wanakilasababu ya kuhakikisha wanawaelekeza vijana wao juu ya umuhimu wa kujikita katika shughuli za uzalishaji mali.

“Vijana hawa wacheza kamali wamekuwa wakikusanyika katika kijiji hiki kutoka vijiji jirani vya Mahenge, Unango, Mkumbi, Litembo na Mundeki”, alisema Komba.

Alisema kuwa pamoja na kucheza mchezo wa kamali pia vijana hao hujiingiza kwenye vitendo vya utumiaji wa madawa ya kulevya ikiwemo uvutaji wa bangi hali ambayo huchangia kudhoofisha nguvu kazi hii muhimu kwa maendeleo ya taifa.

Aliwataka wazazi, viongozi wa Serikali na wanasiasa kushirikiana pamoja kukemea jambo hili linaloendelea kukua kwa kasi katika kijiji hicho na kwamba, wakati umefika kwa vijana kujikita katika shughuli za kilimo ambacho kimsingi kama watafanya hivyo hawatakuwa na muda kwa kupoteza wa kukaa vijiweni.

Mkurugenzi huyo wa vijana pia aliwaasa vijana kujiunga na vyuo vya ufundi ambavyo vimekuwa vikitoa kozi mbalimbali ili hatimaye waweze kupata ujuzi ambao mwisho wa siku watakuwa na uwezo wa kujiajiri wao wenyewe au kuajiriwa.

No comments: