Sunday, December 31, 2017

UZINDUZI KAMPENI ZA UCHAGUZI MDOGO SONGEA: NCHEMBA AWATAKA WANACCM KUVUNJA MAKUNDI



Na Dustan Ndunguru,     
Songea.

NAIBU Katibu Mkuu mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Mwigulu Nchemba amewataka wanachama wa Chama hicho jimbo la Songea mjini Mkoani Ruvuma, kuvunja makundi yaliyojitokeza wakati wa mchakato wa kura za maoni ili kuweza kukirahisishia ushindi CCM katika uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika Januari 13 mwaka huu.

Pia amewataka wananchi wa jimbo hilo kutofanya makosa kupigia kura upinzani kwani kitendo hicho huenda kikasababisha maendeleo waliyofikia kudumazwa kutokana na kudaiwa kuwa na uwezo mdogo wa kuongoza walionao baadhi ya viongozi wa kutoka kambi pinzani.

Mwigulu alisema hayo jana alipokuwa kwenye uzinduzi wa kampeni za uchaguzi mdogo wa Ubunge uliofanyika kwenye viwanja vya Kibulang’oma kata ya Lizaboni mjini hapa.


Kampeni hizo zilihudhuriwa na wanachama wa Chama cha mapinduzi wakiwemo na viongozi mbalimbali na wananchi.

Alisema kuwa wakati wa mchakato wa kura za maoni katika jimbo hilo walijitokeza wanachama 20 kuomba nafasi hiyo, hivyo ni dhahiri kulikuwa na makundi sawa ambayo hivi sasa yanapaswa kuungana pamoja ili kukipa ushindi chama hicho kwa kumnadi kwa nguvu zote mgombea Dokta Damas Ndumbaro.

Alisema kuwa kama makundi ndani ya chama hayatatoweka kutakuwa na uwezekano mkubwa wa kutoa mwanya kwa wapinzani kushinda jambo ambalo halipaswi kupewa nafasi katika jimbo hilo na kwamba CCM ndicho chama pekee chenye dhamira ya dhati ya kuwaletea wananchi wake maendeleo kutokana na kuwa na sera nzuri zisizokuwa na ubaguzi.

Naye mgombea ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya Chama hicho, Dokta Ndumbaro aliomba kura kwa kusema kuwa endapo atachaguliwa kuongoza jimbo hilo atahakikisha anatekeleza kwa vitendo yale yote ambayo yaliahidiwa na mtangulizi wake marehemu Leonidas Gama na kwamba anafahamu wananchi  wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo zinapaswa kupatiwa ufumbuzi ikiwemo elimu, barabara, maji, afya na soko la mazao yao.

Dokta Ndumbaro alisema kuwa changamoto zilizopo kwenye sekta ya kilimo hususan masoko ya mazao ya wakulima chama pekee kinachoweza kutatua kero hizo ni CCM.

No comments: