Tuesday, December 19, 2017

MALORI KAMPUNI YA YARA YAKAMATWA YAKITUHUMIWA KUPAKIA KOKOTO ZA KIJIJI CHA MCHOMORO NAMTUMBO



Na Dustan Ndunguru,      
Namtumbo.

MKURUGENZI Mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Christopher  Kilungu amekamata watu wakiwa na malori tisa Kampuni  ya YARA na katapila moja lililokuwa likitumika kupakia kokoto kwenye malori hayo, ambazo ni mali ya kijiji cha Mchomoro kata ya Mchomoro wilayani humo.

Kukamatwa huko katika  kijiji hicho ni baada ya Diwani  wa kata hiyo, Kassim Nabeha kupata taarifa kutoka kwa wananchi wake kuwa kuna magari yanapakia kokoto za kijiji  hicho ambazo zilitolewa kama zawadi kwa kijiji cha Mchomoro na Kampuni ya China Railway Seventh Group Company Limited (CRSG) iliyokuwa ikijenga barabara ya  lami kutoka Namtumbo mpaka Tunduru.

Nabeha alipofika katika eneo la tukio na kufanya mahojiano na madereva wa magari hayo ni nani aliyewapatia kibali cha kupakia kokoto hizo ambapo alipewa majibu ya kubabaisha na hatimaye alilazimika kuwasiliana na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Kilungu na hatimaye waliweza kuchukua hatua.


Mkurugenzi huyo aliweza kuchukua hatua kwa kutoa taarifa Polisi ambapo waliambatana na kwenda katika eneo la tukio na kufanikiwa kukamata magari ya Kampuni ya YARA na kuyafikisha Kituo kikuu cha Polisi wilayani  Namtumbo.

Kwa  mujibu  wa maelezo ya diwani huyo alimthibitishia Mkurugenzi mtendaji wa wilaya hiyo kuwa kokoto hizo zilitolewa na Kampuni ya CRSG kwa kijiji cha Mchomoro na kuongeza kuwa sio kokoto pekee bali walipewa Pampu ya maji ya kisima cha samaki, nyumba ya bati ya walinzi, mbao na nguzo za kufunga taa za umeme.

Diwani Nabeha alimwambia Mkurugenzi huyo kuwa mara baada ya kukabidhiwa kokokoto hizo baraza la maendeleo la kata lilipitisha na kukubaliana kwamba kokoto hizo, zitumike katika ujenzi wa zahanati  za vijiji vya kata ya Mchomoro ambapo hivi sasa kijiji cha Masuguru na Mchomoro wanaendelea na ujenzi wa zahanati hizo na kwamba kokoto hizo ndio tegemeo katika kukamilisha kazi ya ujenzi huo.

Msemaji wa madereva waliokuwa wakiendesha magari hayo ambayo yalikuwa yakipakia kokoto hizo, aliyefahamika kwa jina moja maarufu la Mndende alisema kuwa  wao hawafahamu  utaratibu uliotumika kwenda kuchukua kokoto hizo ambapo wao walipata maelekezo kutoka kwenye kampuni ya YARA kwenda kupakia kokoto hizo.

Hata hivyo malori  hayo yalipelekwa Kituo cha Polisi wilayani Namtumbo kwa ajili ya kuchunguza kosa la uvamizi wa kuchukua kokoto za kijiji cha Mchomoro bila idhini ya Serikali ya kijiji au Ofisi ya Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo.

No comments: