Monday, December 11, 2017

MPEPO ATAFUTWA NA POLISI KWA KUSABABISHA MAUAJI TUNDURU

Na Muhidin Amri,   
Tunduru.

DEREVA anayejulikana kwa jina la Dastan Mpepo aliyekuwa akiendesha gari aina ya Nissan Forward lenye namba za usajili T 779 ASC anatafutwa na Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma kwa tuhuma ya kusababisha mauaji Wilayani Tunduru mkoani humo.

Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Gemini Mushi alisema kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 9 mwaka huu majira ya saa 3:30 usiku baada ya dereva huyo kugongana uso kwa uso na mwendesha Pikipiki aliyetambuliwa kwa jina la Yusto Seleman Mtega (43) ambaye ni Meneja wa Kampuni ya ulinzi Komesha Security iliyopo Tunduru mjini.

Kamanda Mushi alifafanua kuwa baada ya Meneja huyo kugongwa na gari hilo katika eneo la Kona ya mbwa iliyopo mjini hapa dereva alitekeleza gari lake na kutokomea kusikojulikana.

Alisema kuwa Mtega kabla ya kukutwa na umauti alikuwa akiendesha Pikipiki hiyo aina ya Sunlg akielekea nyumbani kwake ambako anaishi katika mtaa wa Biasi.

Kamanda Mushi amewataka wanachi ambao watapata taarifa ni wapi dereva Mpepo amekimbilia watoe taarifa kwa Jeshi la Polisi ili waweze kumpata mtuhumiwa huyo na sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Kwa upande wake akizungumzia taarifa za tukio hilo Meneja msaidizi wa kampuni hiyo, Said Kaondo Issa alisema kuwa marehemu aligongwa katika barabara ya Tunduru-Namtumbo katika eneo la mtaa wa Kona ya mbwa wakati anaelekea nyumbani kwake muda mfupi baada ya kukamilisha majukumu yake ya kazi ya kuwasambaza askari wa kampuni hiyo kwenda katika maeneo ya malindo ambako wanafanya kazi.

Alisema kufuatia hali hiyo tayari amekwisha wasiliana na Mkurugenzi wa kampuni kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa kusafirisha mwili wa marehemu kuelekea katika kijiji cha Lupanga kilichopo Wilaya ya Ludewa kwa ajili ya taratibu za mazishi.

Dokta Titus Tumbu ambaye ni Mganga aliyeufanyia uchunguzi mwili wa marehemu huyo, alisema kuwa chanzo cha kifo hicho kilitokana na ubongo wake kupata mkandamizo na kupasuka kwa fuvu la kichwa baada ya kugongwa na gari hilo.

Pia Dokta Tumbu aliongeza kuwa katika tukio hilo marehemu aliumia vibaya kwa kuvunjika miguu yote miwili pamoja na mkono wa kushoto.

No comments: