Thursday, December 7, 2017

VIONGOZI RUVUMA WATAKIWA KUTOWAKIMBIA WAANDISHI WA HABARI

Na Kassian Nyandindi,   
Songea.

WITO umetolewa kwa Viongozi wa taasisi za Serikali na binafsi mkoani Ruvuma, kuwa karibu na Waandishi wa habari pale wanapohitaji ufafanuzi wa mambo muhimu ya maendeleo kwa faida ya wananchi, ikiwemo kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha imeelezwa kuwa viongozi hao waache tabia ya kumwona mwandishi wa habari kama adui, badala yake wanapaswa kuona ni marafiki na kutoa ushirikiano wa kutosha katika kazi zao za kila siku.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme alisema hayo juzi wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wa mkoa huo katika Ikulu ndogo mjini Songea.

Alisema kuwa kumkwepa mwandishi wa habari ni kitendo ambacho hakikubaliki katika jamii na kwamba aliongeza kuwa, hategemei kusikia hasa kwa wakuu wa taasisi za Serikali mkoani humo wakifanya vitendo vya kutoshirikiana na waandishi hao katika kujenga maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla.

“Niwapongeze wale mnaoibua maovu sisi Serikali tupo tayari kuyafanyia kazi, Ofisi yangu ipo wazi muda mwingi nawakaribisheni mje tushirikiane katika kuutangaza mkoa wetu, ili malengo ya Serikali ya awamu ya tano yaweze kuwafikia ipasavyo wananchi wake”, alisema.

Vilevile aliwataka wanahabari kuwa karibu na jamii katika kuisaidia Serikali kuibua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi.

Alisisitiza kuwa wanahabari katika mkoa huo wanapaswa kufuata maadili yao ya taaluma kwa kuzingatia uaminifu, weledi na uzalendo na kuwa tayari kujituma sehemu yoyote ile pasipo kuvunja sheria za nchi.

“Tunapoandika habari zetu basi tuuvae uzalendo zaidi kwa sababu amani, utulivu na maendeleo tuliyonayo ni yetu sote tukiharibu ni sisi tutakuwa tumeharibu kalamu yetu, mkono wetu na macho yetu isiwe ni chanzo cha upotoshaji katika kufanya kazi zetu za kila siku na pia tujiepusha na watu wenye nia mbaya ambao huwatumia ninyi waandishi kwa namna moja au nyingine kupotosha umma kwa maslahi yao binafsi”, alisisitiza Mndeme.

No comments: