Thursday, December 7, 2017

RC RUVUMA AWATAKA WAVULANA KUACHA VITENDO VYA KUWAHADAA WATOTO WA KIKE

Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme akisisitiza jambo wakati alipokuwa akizungumza juzi na waandishi wa habari (Hawapo pichani) Ikulu ndogo iliyopo mjini Songea, mwanzoni upande wa kushoto ni Katibu tawala wa mkoa huo, Hassan Bendeyeko na kutoka upande wa kulia ni Andrew Kuchonjoma ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha waandishi wa habari mkoa wa Ruvuma (RPC). 
Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme ametoa wito kwa wazazi na wananchi wa mkoa huo kupuuza habari zinazosambaa katika mitandao ya kijamii, kwamba amekataza watu wazima mkoani humo marufuku kuitana baby jambo ambalo sio la kweli.

Aidha alifafanua kuwa kauli hiyo inamlenga mwanafunzi wa kike ili aweze kufikia ndoto yake ya kumaliza masomo anapokuwa shuleni, ambapo anapaswa kuvaa magauni manne na asikubali kuitwa baby au mrembo na wavulana ambao huwahadaa kwa lengo la kufanya nao mapenzi na hatimaye kukatisha masomo yake.

Hayo yalisemwa juzi na Mkuu huyo wa Mkoa wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ikulu ndogo mjini Songea.


Alisema kuwa kauli hiyo inamaana kwamba, gauni la kwanza linamtaka mtoto wa kike shuleni avae sare zake za shule, gauni la pili avae joho la mahafali, la tatu avae gauni la harusi na la nne ndipo avae gauni la pale anapokuwa na ujauzito.

Mndeme alieleza kuwa mwanafunzi huyo anapovaa gauni la kwanza maana yake anapaswa kuzingatia masomo yake mwanzo hadi mwisho kwa kuhakikisha hawezi kuingia katika vishawishi vya kupata mimba ambavyo vinakatisha ndoto yake ya kuendelea na masomo.

Vilevile kwa gauni la pili alieleza kuwa hapo mtoto wa kike anakuwa tayari amepevuka na kuweza kuvaa gauni la tatu ambalo ni la harusi baada ya kupa mume.

“Kauli mbiu hii nimekuwa nikiitumia mara kwa mara na imekuwa ikinisaidia katika kupambana na mimba za utotoni hasa kwa watoto waliokuwa shule na nina uhakika kwa mkoa huu wa Ruvuma itanisaidia sana hivyo wanafunzi wa kike wasikubali kushawishiwa na wavulana kwa kuitwa baby na hatimaye kukatisha masomo yao”, alisema Mndeme.

Aliongeza kuwa amesikitishwa na baadhi ya watu ambao wamekuwa wakitafsiri kauli hiyo tofauti na alivyosema na kuongeza kuwa malengo yake makuu ni kupambana na mimba za utotoni hasa kwa watoto wa kike ambao wapo shuleni.

“Kitendo cha wanafunzi wa kike kuitwa baby kikiachwa bila kukemewa miongoni mwa jamii kinaleta athari mbaya katika makuzi ya mtoto wa kike na maendeleo yake kielimu anapokuwa shuleni, wanaume wenye nia mbaya wamekuwa wakiwahadaa watoto hawa eti anampenda huku akimuita baby na baada ya huingia katika vishawishi na kumsababishia ujauzito na ndiyo inakuwa mwisho wa ndoto ya mtoto kufikia malengo yake kielimu”, alisema.

Alibainisha kuwa wakati mwingine vitendo hivyo husababisha watoto hao kupata maambukizi ya Virusi vya ugonjwa wa ukimwi na kusababisha vifo kwa sababu ya kuzaa katika umri mdogo.

Alisisitiza kuwa Serikali ya awamu ya tano itaendelea kupambana na watu wenye nia mbaya wanaoshawishi watoto hao katika umri wa kwenda shule kukatisha masomo yao baada ya kupata ujauzito.

Pamoja na mambo mengine, Novemba 8 mwaka huu Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Mndeme alitoa kauli hiyo ya kuitaka jamii iache kuwaita watoto wa kike baby wakati alipokuwa hivi karibuni katika ziara yake ya kikazi wilayani Namtumbo mkoani humo.

No comments: