Monday, December 18, 2017

WANANCHI MKUMBI HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA WAJENGA SHULE YA MSINGI



Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

WANANCHI wanaoishi katika kijiji cha Mkumbi kata ya Mkumbi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamejitokeza na kushirikiana pamoja kujenga shule ya msingi Magingo iliyopo kwenye kata hiyo ikiwa ni jitihada yao na lengo la kuwaondolea adha wanayoipata hivi sasa watoto wao kwenda kusoma umbali mrefu.

Aidha imefafanuliwa kuwa ujenzi wa shule hiyo unatokana pia na watoto wanaosoma katika shule ya msingi Lugari katika kata hiyo kuwa wengi na vyumba vya madarasa havitoshelezi.

Benuard Komba ambaye ni Mwenyekiti wa kijiji hicho alisema kuwa ujenzi huo ni muunganiko wa nguvu za wananchi kwa lengo la kuweza kumaliza changamoto wanayoipata watoto wao kutembea umbali mrefu wa kilometa mbili kufuata elimu.


Alisema kuwa katika kipindi cha masika wanafunzi wamekuwa wakipata shida kutembea kwa miguu kwenda shuleni hivyo waliona ni vyema katika kumaliza kero hiyo wajenge shule nyingine karibu na makazi yao ili watoto waweze kupata elimu kwa urahisi.

“Tuliona ni vyema kujenga shule hii, watoto darasani wanakuwa zaidi ya 100 tunajenga tuweze pia kupunguza wingi wa watoto kurundikana darasani na kumrahisishia hata mwalimu anapokuwa kwenye vipindi vya masomo aweze kufundisha kwa urahisi”, alisema Komba.

Ujenzi wa shule hiyo ambao ulianza Agosti 21 mwaka huu hivi sasa tayari wameweza kufikia hatua ya kukamilisha jengo moja lenye vyumba viwili vya madarasa na ofisi moja ya walimu.

Vilevile mwandishi wetu ameshuhudia ujenzi wa jengo la pili ukianza huku taratibu za ujenzi wa vyoo na nyumba za walimu ukiendelea kufanyika ambapo mara ujenzi huo utakapokamilika ikifikapo Januari mwaka huu wanatarajia watoto waweze kuanza kusoma katika majengo hayo.

Naye Gabinus Kapinga ambaye ni mwananchi wa kijiji cha Mkumbi alisema kuwa wanaiomba Serikali iendelee kuwaunga mkono ili waweze kufikia hatua nzuri ya kuweza kukamilisha haraka ujenzi wa majengo hayo na watoto wao waweze kusoma mahali pa zuri.

Kadhalika akizungumzia hilo Kaimu Afisa mipango wa wilaya ya Mbinga, Zainabu Mfinanga alieleza kuwa ujenzi huo wanashirikiana na halmashauri ya wilaya hiyo, ambapo wamekuwa wakiwapatia vifaa vya kiwandani ili kuweza kufikia hatua nzuri ya kukamilisha kazi hiyo ya ujenzi.

No comments: