Wednesday, January 3, 2018

LHRC YAITAKA SERIKALI KUHESHIMU KATIBA

Na Mwandishi wetu,
Dar es Salaam. 

KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeviomba vyombo vya kimataifa vinavyohusika na uangalizi wa haki za binadamu kuingilia kati suala la uhuru wa kujieleza nchini.

LHRC pia imetaka Serikali kuheshimu Katiba kwa kutoingilia uhuru wa kujieleza.

Kauli hiyo imetolewa leo siku moja baada ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuvitoza faini vituo vya televisheni vya ITV, Azam Two, Startv, Channel Ten na EATV kwa kukiuka kanuni ya maudhui ya mwaka 2005.


Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dokta Hellen Kijo-Bisimba alisema kuwa uamuzi wa kutozwa faini vituo hivyo ni ukandamizaji wa uhuru wa vyombo vya habari wa kutoa taarifa kwa jamii na hasa zinazoikosoa Serikali.

"Serikali ikubali kuyasikiliza mazuri na mabaya na kuyatumia maoni ya wananchi, vituo hivi vimetozwa faini kwa sababu vimetoa taarifa ya tathmini iliyotolewa na LHRC kuhusu uchaguzi mdogo wa madiwani uliofanyika Novemba mwaka jana”, alisema.

Dokta Kijo–Bisimba aliongeza kuwa, “Kwetu tunaona hili si sawa na tunaona mambo haya yanazidi kuongezeka, Serikali kupitia Jeshi la Polisi wamekuwa wakitumia neno uchochezi kuminya uhuru wa mawazo na kujieleza”.

Kutokana na hilo, LHRC ipo tayari kuungana na wadau ambao wako tayari kwenda mahakamani kuomba tafsiri ya neno uchochezi na baadhi ya vifungu vya kanuni ya maudhui.

Dokta Kijo – Bisimba  alieleza kuwa LHRC imeanzisha harambee kuchangia gharama kuvisaidia vyombo vya habari vilivyokumbwa na adhabu hiyo.

No comments: