Saturday, January 27, 2018

MADABA WAJIVUNIA MAFANIKIO UZALISHAJI MICHE YA KOROSHO



Na Kassian Nyandindi,
Madaba.

HALMASHAURI ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, katika msimu wa mwaka huu inatarajia kupanda miche ya zao la Korosho 55,020 sawa na ekari 1,965 ya zao hilo ikiwa ni mkakati uliojiwekea Halmashauri hiyo katika kuongeza vyanzo vyake vya mapato kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.  

Shafi Mpenda ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Madaba alisema kuwa pamoja na jitihada hizo Serikali kuu kupitia Bodi ya korosho Tanzania, imekuwa ikisaidia kuendeleza zao hilo kwa kuleta mbegu bora, miche iliyobebeshwa, vifaa vya kitalu, viuatilifu na kufanya mafunzo kwa wakulima wa zao hilo.

Mpenda alieleza kuwa tayari miche hiyo wamekwisha anza kusambaza kwa wakulima katika vijiji mbalimbali hasa vile vyenye hali ya hewa inayostawi vizuri korosho ikiwemo kijiji cha Mbangamawe, Ifinga, Ngadinda, Gumbiro, Lutukila, Mtyangimbole, Magingo, Kipingo na Mahanje.


Alisema kuwa mbali na mikakati waliyonayo katika kuendeleza kilimo cha zao hilo Halmashauri yake kwa kushirikisha maafisa ugani waliopo vijijini imejitahidi kusimamia mazao mengine ya biashara kama vile kahawa na tangawizi huku upande wa mazao ya chakula ikiwemo mahindi, mpunga, maharage, soya, karanga na mazao ya bustani ambayo hulimwa kwa wingi na kufanya hali ya chakula kuwa nzuri wilayani humo.

Katika kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) alisema kijiji cha Mbangamawe kimefanikisha kuanzisha Chama cha ushirika cha mazao, ambacho kazi yake kubwa ni kukusanya  mazao toka kwa wakulima na kutafuta masoko, pembejeo za kilimo na kuziuza kwa wakulima ambo ni wanachama na wale wasiokuwa wanachama.

Mpenda aliongeza kuwa pamoja na  jithada hizo za wakulima na Serikali katika kuendeleza zao la korosho wanakabiliwa na changamoto ya upungufu wa mbegu  za korosho zinazotolewa na Bodi husika kwani katika msimu wa mwaka huu mahitaji yalikuwa ni miche 130,000 lakini miche iliyopatikana ni 55,020.

Mbali na mbegu kuwa pungufu pia upatikanaji wa pembejeo umekuwa ni tatizo kama vile mbolea hazitoshelezi kwani mahitaji ya wakulima yamekuwa makubwa.

No comments: