Wednesday, January 24, 2018

RAIS MAGUFULI AMTUMIA SALAMU ZA RAMBIRAMBI JAJI MKUU WA TANZANIA

Rais Dokta John Pombe Magufuli.


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Jaji Mkuu wa Tanzania, Ibrahim Juma kutokana na kifo cha Jaji mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Robert Kisanga.

Jaji Kisanga alifariki dunia jana Jumanne Januari 23 mwaka huu katika Hospitali ya Regency Jijini Dar es Salaam.

Taarifa ya Ikulu iliyotolewa leo Januari 24 mwaka huu imemnukuu Dokta Magufuli akisema kuwa Jaji Kisanga atakumbukwa kwa mchango wake alioutoa kwa Taifa hili wakati wote wa utumishi wake.


Dokta Magufuli alisema kuwa utumishi wa Jaji Kisanga ulijaa umakini, uchapakazi, uzalendo na ushirikiano kwa wengine, mambo ambayo yalimwezesha kupata mafanikio makubwa.

“Sote tunafahamu kazi nzuri alizofanya akiwa katika majukumu ya kitaifa, mchango wake katika kuijenga taaluma ya uanasheria baada ya uhuru na uanzishaji wa Mahakama ya Rufani baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1977, kwa hakika mchango wake hautasahaulika”, alisema.

Kadhalika alimuomba Profesa Juma kufikisha rambirambi hizo kwa familia ya Jaji Kisanga, majaji na wanasheria wote, ndugu, jamaa na marafiki walioguswa na msiba huo.

Hata hivyo amewaomba wafiwa kuwa na moyo wa subira, uvumilivu na ustahimilivu katika kipindi hiki cha majonzi.

No comments: