Monday, January 29, 2018

VIWAVI JESHI WAHARIBIFU WA MAZAO WADHIBITIWA SONGEA



Na Kassian Nyandindi,    
Songea.

WADUDU aina ya viwavi jeshi (Fally arm worms) ambao wameingia katika Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, tangu mwezi Mei mwaka jana mpaka sasa wamefanya uharibifu mkubwa wa mazao na wataalam husika wamefanikiwa kuwadhibiti kwa asilimia 95.

Afisa Kilimo wa Halmashauri ya Manispaa hiyo, Zawadi Nguaro alisema kuwa viwavi hao wana uwezo wa kushambulia aina 80 ya mazao yakiwemo mahindi, miwa na mtama na kwamba tangu walipoingia katika Manispaa hiyo walianza kwa kushambulia nyasi.

Alisema kuwa wadudu hao waligundulika mwishoni mwa mwezi Desemba 2017 wakiwa wameshambulia Hekta zaidi ya 1,000 za mahindi, ambapo wadudu hao hutoboa majani ya mahindi na kuchana kama kamba na kwamba wana uwezo wa kushambulia kwa kasi kubwa iwapo hawadhibitiwi haraka.


Anayataja maeneo ambayo yaliathirika zaidi na wadudu hao kuwa ni kata ya Lilambo ambayo Hekta 299 ziliharibiwa, Subira (250), Tanga (180), Mletele (100), Ruhuwiko (120) Mshangano (50), Matogoro (10), Ruvuma (26), Seedfarm (20) na Mateka Hekta tano.

Nguaro aliongeza kuwa tangu walipogundulika wadudu hao idara ya kilimo imekuwa ikitoa elimu na ushauri juu ya namna ya kupambana nao, ikiwemo matumizi ya viuatilifu vya kukabiliana na ugonjwa huo ambapo wakulima wamekubali ushauri na kununua viuatilifu hivyo hatimaye kufanikiwa kupunguza tatizo hilo kwa kiwango kikubwa.

Anavitaja viuatilifu ambavyo vilikuwa vikitumika katika kukabiliana na wadudu hao kuwa ni MUPA FORCE 720 EC, AGROCRON 720EC, PROTRIN 600 EC, PROSPER 720 EC na DUDUBA 720 EC.

No comments: