Sunday, November 18, 2012

BALOZI KAGASHEKI ALIA NA WAWINDAJI HARAMU TUNDURU

Bunduki zilizokamatwa katika Oparesheni ya kukamata wawindaji haramu wilayani Tunduru.(Picha na Steven Augustino)


Na Steven Augustino,


Tunduru.

WAZIRI wa Maliasili na Utalii Balozi Hamisi Kagasheki ameadhimia
kupeleka Bungeni juu ya kubadilisha sheria na kuongeza adhabu
kwa watuhumiwa wa makosa ya jinai za uhujumu uchumi ambavyo vimekuwa vikifanywa na wawindaji haramu.

Hali hiyo imefuatia serikali baada ya kubaini kushamiri kwa vitendo vya uhalifu na ujangiri, kufuatia oparesheni maalumu iliyofanyika wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, na kufanikiwa kukamata mali zenye thamani ya shilingi milioni 618.408.

Waziri Kagasheki alisema kuwa kuanzia sasa
serikali haitawavumilia na kuwaacha wajanja wachache wakiendelea
kujinufaisha kupitia maliasili za taifa hili, na kwamba alisema adhabu za watuhumiwa hao ni vyema ziwe kati ya miaka 40 na 50.

Aidha pamoja na kuwapongeza askari waliofanikisha kukamata kwa mali hizo Waziri Kagasheki alisema kuwa oparesheni hiyo ni endelevu na akatumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi wa wilaya hiyo na maeneo mengine kuendelea kutoa ushirikiano wa karibu, utakaofanikisha kukamatwa kwa wahusika wengine waliokimbia.



Kwa mujibu wa taarifa za oparesheni hiyo miongoni mwa mali zingine
zilizokamatwa katika zoezi hilo ni pamoja na bunduki zaidi ya
300 na risasi 667 na maganda ya risasi 150 zilizobainika kumilikiwa
kinyume cha taratibu.

Mali zingine zilizokamatwa ni pamoja na gari moja aina ya Toyota, Piki piki 4 ambavyo wahusika walivitelekeza na kukimbia kusikojulikana, baada ya kubainika kuwa vilikuwa vimehusika kubeba nyara hizo za serikali.

Aidha katika msako huo pia Mbao 10,183 mti pori zenye dhamani ya shilingi milioni 377,257,000 zilikamatwa huku asilimia 90% ya mbao hizo ni za
mti aina ya mninga.

Akisoma taarifa ya oparesheni hiyo kwa niaba ya Mwenyekiti wa
oparesheni hiyo Bw. Samson Mkasla, mtendaji mkuu wa msako wa kuwakamata wahalifu hao Bw. Emmanuel Kandihabi alisema kuwepo kwa mafanikio hayo makubwa kunatokana na ushirikiano mzuri kutoka kwa viongozi wa serikali na wananchi wa wilaya hiyo.
 

Bw. Kandihabi aliendelea kueleza kuwa tayari silaha zote zitahifadhiwa
Polisi katika kipindi cha miaka miwili na kwamba wamiliki hao pia
ambao wamefungwa kifungo cha nje kwa muda wa miaka miwili watatakiwa kuomba upya baada ya muda huo kwisha.



Akizungumzia taarifa za matukio hayo Bw. Kandiahabi alisema kuwa
katika kipindi hicho walifanikiwa kukamata jumla ya wahalifu 163
wakiwa na vilelezo vya bunduki, risasi, meno ya tembo na viboko, mikia na singa za tembo vyote vikiwa na thamani ya Shilingi bilioni 2,241,147,22.

Alisema katika kipindi hicho pia majalada 123 yalifunguliwa katika
Kituo cha Polisi Tunduru na tayari kesi 55 zimekwisha pelekwa Mahakamani, ambapo kesi 43 zimekwisha tolewa hukumu kwa wahusika kufungwa kati ya kifungo cha miaka 10 na miaka 5 jela huku wengine wakitozwa faini.

Awali akisoma taarifa ya wilaya hiyo kwa niaba mkuu wa wilaya ya
Tunduru Bw. Chande Nalicho kaimu afisa tawala wa wilaya Bw. Manfred Hyera alisema kuwa katika kudhamini maendeleo ya idara hiyo tayari
wilaya hiyo, imetenga kiasi cha shilingi 38,875,097/71  na halmashauri
ya wilaya kwa ajili ya kutekeleza shughuli za maliasili katika kipindi cha mwaka 2012/2013.

Kikosi hicho kinashirikisha maafisa kutoka katika majeshi ya Polisi, Jeshi la wananchi, usalama wa taifa, Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa(PCCB), Magereza na kuwashirikisha maafisa kutoka mamlaka ya Mapato(TRA) na kuongozwa na Kamanda mstaafu wa jeshi la Polisi Bw. Venance Tossi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kamanda Tossi alisema, oparesheni hiyo ni ya pili kufanyika na kueleza kuwa iliwahi kufanyika mwezi Julai katika wilaya ya Liwale mkoani Lindi.

No comments: