Thursday, November 29, 2012

GAUDENCE KAYOMBO AWATAKA WANANCHI WAKE KUJITUMA KATIKA SHUGHULI ZA KIMAENDELEO


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WANANCHI wa jimbo la Mbinga Mashariki mkoani Ruvuma, wametakiwa kuendelea kujituma katika shughuli mbalimbali za kimaendeleo ili waweze kuondokana na umaskini, ambao umekuwa ukiitesa jamii miongoni mwao.

Mbunge wa jimbo hilo Bw. Gaudence Kayombo(Pichani) alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na Mwandishi wa habari hizi, juu ya mikakati mbalimbali ya kusukuma maendeleo katika jimbo lake.

Bw. Kayombo alisema kuwa anafurahishwa na wananchi wa jimbo la Mbinga Mashariki, kwamba wengi wao wamekuwa wakijituma katika shughuli za maendeleo hasa katika nyanja ya kilimo cha mazao mbalimbali.

Alisema hivi sasa amekuwa akihamasisha wananchi hao kuunda vikundi vya kilimo cha mazao mchanganyiko yakiwemo mahindi, maharage alizeti na mpunga lengo ni kuwafanya waweze kuwa na kipato ambacho kitawasaidia hata kupeleka watoto wao shule.

“Hivi sasa tupo katika mchakato wa kusajili vikundi 60 vya mazao mchanganyiko changamoto niliyonayo sasa mwitikio ni mkubwa mno, na mimi nimefurahishwa sana na wananchi wangu kupokea jambo hili kwa mikono miwili hivyo usajili huu utakapokamilika tutafuta masoko ili waweze kuuza mazao yao kwa bei nzuri”, alisema.

Alifafanua kuwa usajili wa vikundi hivyo utasaidia hata kwa kikundi husika kiweze kutambulika kisheria serikalini na kwa taasisi binafsi, zikiwemo benki ambazo zitaweza kuwapa mikopo ya kuendeshea shughuli zao za kilimo.

Kadhalika aliongeza kuwa amekwisha fanya mawasiliano na shirika la VECO na AGRI CORD yaliyopo Ubelgiji, kwa ajili ya kuweza kusaidia vikundi vya kilimo cha mazao mchanganyiko wilayani Mbinga, kwa kuwapa utaalamu wa kilimo bora na hata msaada wa kifedha kwa ajili ya kuendeshea shughuli za kilimo.

Pamoja na mambo mengine, awali alieleza kuwa ameweza kuhamasisha pia wakulima wa zao la kahawa wilayani humo, kuunda vikundi vya wakulima wa kahawa ambapo jumla vipo 64 ambavyo vimesajiliwa kisheria na sasa vimekwisha anza kazi ya kuuza kahawa yao katika msimu wa mwaka huu wa mavuno ya zao hilo.

“Tumekwisha peleka tani 140 za kahawa zipo pale Makambako kwa ajili ya kuuza mnadani, na mimi nimezungumza na watu wa Korea kusini na Israel ambako kuna masoko makubwa wapo tayari kununua kahawa yetu, kupitia vikundi hivi vilivyosajiliwa”, alisema Bw. Kayombo.

Hata hivyo alieleza kuwa kufikia mwaka 2014 katika wilaya ya Mbinga kutajengwa kiwanda cha usindikaji wa kahawa, lengo likiwa ni kukuza uchumi wa wilaya hiyo na taifa kwa ujumla.

“Nimeanza kuzungumza na wafadhili ambao watasaidia katika ujenzi huu, kuanzia mwakani mwezi Januari watakuja kwa ajili ya kuanza upembuzi wa awali juu ya kazi hii”, alisema.

No comments: