Friday, November 23, 2012

MADEREVA PIKIPIKI TUNDURU WALISHUTUMU JESHI LA POLISI


















Kamanda wa polisi mkoa wa Ruvuma, Bw. Deusdedith Nsemeki.


Na Steven Augustino,
Tunduru.

Madereva wa pikipiki maarufu kwa jina la Boda boda wameaswa kuunganisha nguvu zao na kuisaidia serikali kwa kutoa taarifa zitakazosaidia kudumisha amani na utulivu.

Pamoja na utekelezaji wa maadhimio hayo pia madereva hao wamehimizwa kuwa na leseni za udereva pamoja na kutumia fursa na asilimali zilizopo katika maeneo yao, ili kujiletea maendeleo.

Mwito huo umetolewa na Mkuu wa wilaya ya Tunduru Bw. Chande Nalicho alipokuwa akizungumza na Madereva hao katika kikao kilichofanyika ukumbi wa Klasta mjini hapa, na kuongeza kuwa endapo wataendelea kujitenga hawatapata mafanikio huku wakihatarisha hali ya amani ya taifa lao, kwani taarifa zao pia zitasaidia kulinda maisha yao na jamii nyingine kwa ujumla.

Akifafanua taarifa hiyo Bw. Nalicho alisema kuwa ili wapate mafanikio kupitia kazi wanazozifanya wanapaswa kutoa ushirikiano kwa kuwataja wahalifu, ambao ni kati ya wateja ambao kwa namna moja au nyingine huwasafirisha na kuwapeleka katika maeneo ya uhalifu huku wakiwa
wanafahamu au la.

“ Kazi mnazofanya ni za hatari kwa maisha yenu na jamii inayowazunguka, hivyo tunaomba ushirikiano wenu katika utoaji wa taarifa ili kuisaidia serikali kupambana na vitendo vya uhalifu ambavyo vimekuwa vikisababisha madhara makubwa kwa jamii”, alisema Bw. Nalicho huku akihimiza hata kutoa taarifa kwa kumpigia yeye moja kwa moja kupitia simu namba 0754596536.

Akifafanua matumizi ya fursa za maendeleo Mkuu huyo wa wilaya ya Tunduru aliwataka madereva hao kujiunga katika vikundi na kuanzisha Saccos, ili waweze kulima katika  mabonde ambayo hutiririsha maji kipinda cha mwaka mzima ili waweze kujiletea maendeleo na kuongeza vipato ambavyo vitawawezesha kufikia malengo husika.

“Wilaya yetu ni tajiri kwani inamabonde mengi yanayo tiririsha maji mwaka mzima na yanakubali kulima mazao ya aina mbalimbali, nawaomba myatumie kikamilifu ili kujiletea maendeleo”, alisema.

Aliongeza kuwa takwimu kutoka idara ya kilimo zinaonesha kuwa mbali na asilimia 95 ya wakazi wa wilaya hiyo kutegemea kilimo eneo linalo limwa kwa sasa ni asilimia 21 tu kati ya eneo la hekta 914,000 linalofaa kwa shughuli za kilimo.

Wakiongea kwa nyakati tofauti baadhi ya madereva hao walilishutumu Jeshi la Polisi wilayani humo, kuwa limekuwa likiwanyanyasa kutokana nawakati mwingine kuwakamata na kuwatoza faini bila sababu zozote za msingi.

Walisema hali hii imekuwa ikileta uhasama miongoni mwao na kuwa kikwazo katika ushirikiano huo.

Wakifafanua taarifa hiyo kwa niaba ya madereva hao Bw. Bushiri Said, Mohamed Senjele na Isaa Msamati walisema, kuwa katika kutekeleza vitendo hivyo vya kibabe, dhuluma na uonevu unaofanywa na polisi, wakati mwingine Polisi hao wamekuwa wakiwakamata kwa kutumia mbinu za kupandisha kamba wanazozifunga barabarani na kuwanasa hali ambayo imekuwa ikiwasababishia ajali na maumivu makali.

Akijibu kero hizo Kamanda wa Polisi wa wilaya ya Tunduru SP. Amedeus Tesha, aliwataka madereva hao kutokata tamaa na vitendo hivyo na akawaomba kupeleka malalamiko hayo kupitia simu namba 0754 695784 au 0715695783 na kwa kuwataja askari wenye tabia hizo ili ikidhibitika sheria ifuate mkondo wake.

No comments: