Friday, November 9, 2012

UPINZANI SYRIA KUUNGANA DHIDI YA ASAAD



Rais Bashr Al Assad amesema hayuko tayari kuondoka Syria licha ya upinzani mkali dhidi ya serikali yake.





Baraza la upinzani nchini Syria linakabiliwa na kibarua kigumu kuamua ikiwa litajiunga na makundi mengine ya upinzani ambayo yanaonekana kuwa na msimamo mmoja.
Hatua hii ya upatanishi inalenga kuleta upinzani pamoja na jeshi lililomegeka ili kuunda serikali mbadala kwa ile ya Rais Assad.
Mataifa ya ghuba pamoja na nchi za Magharibi, zimekuwa zikishinikiza kuwepo mfano wa chama kimoja ambacho kitaweza kusaidia kurahisisha huduma za misaada na hata kijeshi kwa raia.

Wakati huohuo, mashirika ya Umoja wa Mataifa, yako mjini Geneva kujadili harakati za kutoa misaada nchini Syria.


Kurahisisha uwezo wa wafanyakazi wa mashirika ya misaada kutoa misaada itakuwa juu kwenye ajenda ya vyama hivyo katika mkutano wa sita kuhusu maswala tya kibinadamu ambao unaleta pamoja mashirika ya Umoja wa Mataifa na nchi wanachama.

Serikali ya Syria imetatiza sana uwezo wa mashirika ya misaada kuendesha shughuli zao nchini humo.

Harakati za mapinduzi dhidi ya serikali ya Rais Assad zimeendelea kukumbwa na ghasia tangu zianze mwezi Machi mwaka jana.

Wanaharakati wanakadiria kuwa zaidi ya watu 35,000 wameuawa katika vita hivyo. Umoja wa mataifa nao unasema kuwa takriban watu milioni 1.2 wameachwa bila makao huku wengine zaidi ya milioni mbili wakihitaji msaada. (BBC News)

No comments: