Wednesday, November 7, 2012

WANAOENDELEZA MAKUNDI CCM KUKALISHWA KITAKO

 Katibu mwenezi wa chama cha mapinduzi mkoani Ruvuma Bw.  Benedict Ngwenya akizungumza na vyombo mbalimbali vya habari leo mkoani humo(hawapo pichani) katika ofisi za chama hicho mjini Songea, kulia ni katibu wa umoja wa vijana (UVCCM) wa mkoa  Bi. Mwajuma Rashid na kushoto Mwenyekiti CCM mkoani Ruvuma Bw. Oddo Mwisho.





Na Dustan Ndunguru,
Songea.

MWENYEKITI wa chama cha mapinduzi(CCM) mkoa wa Ruvuma Bw. Oddo Mwisho amesema, mwanachama wa chama hicho ambaye ataendekeza makundi kwa lengo la kukigawa chama na wanachama kwa ujumla, atachukuliwa hatua kali kulingana na taratibu za chama ikiwemo kukalishwa kitako katika vikao halali.

Bw. Mwisho alisema kinachotakiwa sasa ni wanachama wenyewe kuwa na maadili mema na sio kuendeleza malumbano yasiyokuwa ya msingi.

Hayo alisema wakati alipokuwa akizungumza na vyombo mbalimbali vya habari mjini Songea, huku  akifafanua kwamba hivi sasa chama hicho kimekuwa kikiwaelekeza wanachama wake kote nchini juu ya umuhimu wa kuyaondoa makundi yaliyotokana na uchaguzi kwa malengo ya kukijenga chama.

“Makundi katika chaguzi mbalimbali za chama lazima yawepo, kila kundi linakuwa na mgombea wake ambaye linamuunga mkono hivyo kinachotakiwa mara baada ya kukamilika kwa uchaguzi na viongozi kupatikana,  linatakiwa libaki kundi moja tu ambalo linakijenga chama kwa mazuri”, alisema.

Hata hivyo alieleza kuwa hatarajii makundi kuendelea kuwepo mkoani Ruvuma, badala yake anaimani mshikamano taendelea kudumu wakati wote.

Kadhalika aliongeza kuwa baada ya kukamilika kwa chaguzi mbalimbali za chama, hivi sasa wanajipanga kushinda chaguzi zijazo za serikali, ambapo kwa kuanzia wanayomatarajio makubwa ya kuibuka na ushindi mkubwa katika uchaguzi wa serikali za mitaa, hivyo mafanikio hayo yatafikiwa pakiwa hakuna makundi yanayosigana ndani ya chama.

Aidha Bw. Mwisho alisema moja ya mkakati ambao wamejiwekea kwa sasa ni kuhakikisha wanaanzisha madarasa ya itikadi, ambayo yatatumika kuwapa elimu ya siasa wanachama wake kabla hawajakubaliwa kujiunga kama wanachama na kwamba mkoa huo unao makada wengi ambao watawatumia kwenda kwenye mashina, tawi na kata kutoa elimu hiyo.

"Hapo awali kulikuwa na madarasa hayo ambayo kimsingi yalikuwa msaada mkubwa kwa chama chetu, hapa kwetu tumeamua kwa dhati kuyarudisha kwani yatatoa mwongozo kwa wanachama wetu watakaoomba kujiunga na chama chetu", alisema Bw. Mwisho.

Pamoja na mambo mengine aliwashukuru wananchi wa kata za Mpepai wilayani Mbinga na Mletele wilaya ya Songea, kwa kuwachagua wagombea wa chama hicho katika uchaguzi mdogo wa udiwani uliofanyika Oktoba 28 mwaka huu.

No comments: