Friday, November 23, 2012

CWT YALALAMIKIA UCHELEWESHAJI WA MALIPO YA WANACHAMA WAKE






 Rais wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Bw. Gratian Mukoba.(Picha IPP MEDIA)






Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHAMA cha Walimu Tanzania (CWT) Wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, kimelalamikia ucheleweshaji wa malipo ya wanachama wake na kudai kuwa hali hiyo inawafanya wanachama hao kuishi katika maisha ya kuwa omba omba.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo jumla ya shilingi 120,423,080 zinazo daiwa na walimu 111  wa wilaya hiyo, yakiwa ni mapunjo yao ya mishahara yaliyolimbikizwa kuanzia mwaka 2009.

Katibu wa chama hicho Bw. Lazaro Saulo alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea katika ofisini za CWT wilayani humo, na kuongeza kuwa kutokana na hali hiyo pia walimu wengi katika maeneo mbalimbali hivi sasa wanakabiliwa na madeni makubwa ambayo wamekuwa wakikopa kutoka katika asasi za fedha ili kujikimu kimaisha.

Bw. Saulo alieleza kuwa malalamiko hayo yanatokana na ucheleweshaji wa muda mrefu, ambapo wanachama wanayadai na kwamba walianza mchakato wa kuyashughulikia kuanzia mwaka 2009 / 2010 / 2011 yakiwa ni mapunjo ya nyongeza ya mishahara yao baada ya kupandishwa madaraja katika kipindi hicho.

Alisema kinachowashangaza wanachama hao ni serikali kuwabagua na kuwalipa walimu 188 kati ya Walimu 299 waliokuwa wanadai jumla ya deni la shilingi  279,686,900  huku kukiwa hakuna maelekezo yoyote kutoka kwa muajiri wao.

Kufuati hali hiyo wanachama wake wamepata mashaka na kuhisi kuwa huenda wamedhulumiwa, hali iliyo kisukuma chama hicho kuandika barua yenye kumbukumbu namba CWT (W) TDR/DED/38 ya Nov. 20 mwaka huu kwenda kwa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, ili kumkumbusha juu ya madai ya walimu hao.

Aidha Bw. Saulo alitumia nafasi hiyo kuipongeza serikali kwa kufanya malipo  jumla ya walimu 188 ambao walilipwa kiasi cha shilingi 154,263,820 katika malipo yaliyofanyika mwezi Agosti mwaka huu, na kuongeza kuwa endapo walimu hao pia watalipwa haki zao chama kinaamini kuwa hali hiyo itainua ari na kuongeza ufanisi kitaaluma.

Akijibu kero hiyo pamoja na kukiri kupokea barua hiyo Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Tunduru Bw. Robert Nahatta alisema kuwa ofisi yake inayafahamu vizuri madai hayo, na kwamba taratibu zinafanywa ili kuhakikisha kuwa walimu hao wanalipwa haki zao.

"Naomba niwahakikishie kuwa hakuna mtu atakayenyimwa haki yake katika malipo haya”, alisema Bw. Nehatta, na kuongeza kuwa kilichofanyika katika uandishi wa barua hiyo ni uoga tu wa viongozi na wahusika kwenda kuuliza na
kupata majibu sahihi kutoka kwa wahusika.

No comments: