Tuesday, November 6, 2012

CCM YAJIVUNIA USHINDI

Rais Jakaya Kikwete





























Na Dustan Ndunguru,
Songea.
 
CHAMA cha mapinduzi (CCM) mkoani Ruvuma kimesema, kuibuka kwa ushindi wa kishindo katika chaguzi ndogo kwa nafasi za udiwani uliofanyika Oktoba 28 mwaka huu, ni ushahidi tosha kuwa chama hicho kinakubalika tofauti na madai yanayotolewa na wapinzani ambao wamekuwa wakidai hakina mvuto kwa watanzania.
 
Katibu wa CCM wa mkoa huo Bi. Verena Shumbusho alisema kuwa katika uchaguzi huo ambao ulifanyika katika kata za Mletele manispaa ya Songea na kata ya Mpepai iliyopo wilayani Mbinga, wananchi waliwachagua wagombea wa chama hicho kwa kura nyingi baada ya kuridhishwa na sera nzuri sambamba na utekelezaji wa yale ambayo waliahidiwa mwaka 2010.
 
Bi. Verena alisema kuwa ushindi huo ni mwanzo mzuri kwa chama hicho, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea katika chaguzi za serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ambapo kinachotakiwa kwa sasa ni kwa viongozi na wanachama kujipanga vizuri huku wakitakiwa kukanusha taarifa zinazotolewa na wapinzani dhidi ya CCM zenye kulenga kukidhoofisha.
 
Alisema kuwa wakati wote wa kampeni vyama vya upinzani vilikuwa vikitoa maneno mabaya ambayo yalilenga kukidhoofisha chama cha mapinduzi, lakini mwisho wa siku wananchi walifanya maamuzi sahihi yatakayopelekea wasonge mbele kimaendeleo kama walivyoahidiwa katika mikutano ya kampeni ya chama hicho.
 
"Chama chetu kilipitia mabonde na milima katika uchaguzi huo mdogo lakini imani waliyonayo wananchi kwetu waliwachagua wagombea wetu tena kwa kura nyingi, tofauti na dhamira waliyokuwa nayo hawa wenzetu", alisema.
 
Katibu huyo aliwashukuru wanachama, wapenzi na wananchi kwa ujumla kutokana na ushindi huo ambapo alisema kuwa kilichobaki kwa sasa ni kwa madiwani waliochaguliwa kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao ipasavyo ili wananchi waweze kujenga imani kwao na kwa chama cha mapinduzi.
 
Alisema baada ya kukamilika kwa uchaguzi huo mshikamano unapaswa kuwepo baina yao kwa malengo ya kufanikisha utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2010 na kwamba viongozi wa vyama vya upinzani wahakikishe wanahamasisha wafuasi wao kujitokeza kuchangia nguvu zao kwenye utekelezaji wa miradi ya kimaendeleo.
 
"Hata kama wagombea wao hawakuchaguliwa ningewaomba hawa wenzetu wahamasishe wafuasi wao wajitokeze kuchangia nguvu zao katika ujenzi wa miradi pale wanapohitajika kwa sababu watakaonufaika nayo sio wana CCM pekee bali ni wote kwani ilani ya CCM haina ubaguzi", alisema Bi. Verena.
 
                      

No comments: