Tuesday, November 13, 2012

JELA KWA KOSA LA UBAKAJI

Na Dustan Ndunguru,
Tunduru.

MAHAKAMA ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma imemhukumu mkazi mmoja wa kijiji cha Nalasi wilayani humo, adhabu ya kifungo cha miaka 30 kwenda jela pamoja na kuchapwa viboko 10 kwa kosa la ubakaji.

Akisoma hukumu hiyo hakimu mkazi katika mahakama ya wilaya hiyo Bw. Ernest Mgongolo alisema, mahakama hiyo imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka kuwa mshitakiwa Issa Mwichande(27) alimbaka mwanafunzi mwenye miaka 11 wa shule ya msingi Nalasi.

Bw. Mgongolo alisema kuwa mahakama imemtia hatiani na kuhukumiwa adhabu ya kifungo cha miaka 30 kwenda jela, sambamba na kuchapwa viboko kumi ambapo viboko vitano atachapwa wakati wa kuingia na vitano wakati wa kutoka akishamaliza kutumikia kifungo hicho.

Awali mwendesha mashitaka wa polisi Inspekta Minde alidai mahakamani hapo kuwa, mshitakiwa huyo alitenda kosa hilo Oktoba mwaka jana saa za asubuhi nyumbani kwa mwanafunzi huyo.

Wakati huo huo mkazi mmoja wa kijiji cha Lukumbule wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, amehukumiwa na mahakama ya wilaya hiyo, adhabu ya kifungo cha miaka 3 kwenda jela baada ya kupatikana na kosa la kumbaka mwanafunzi wa darasa la saba.

Akisoma hukumu hiyo Hakimu mkazi katika mahakama ya wilaya ya Tunduru Bw. Ernest Mgongolo alisema kuwa mahakama, imeridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka kuwa mshitakiwa Bakari Ismail Bakari(20) alimbaka mwanafunzi wa darasa la saba shule ya msingi Lukumbule.

Hakimu huyo alisema kuwa mahakama imemtia hatiani na kumhukumu adhabu ya kifungo cha miaka mitatu kwenda jela, viboko vitano, faini ya shilingi milioni 3 na kulipa fidia ya shilingi milioni moja.

Awali mwendesha mashitaka wa polisi Inspekta Minde alidai mahakamani hapo kuwa, mshitakiwa Bakari alitenda kosa hilo mwezi Oktoba mwaka huu, saa za asubuhi wakati mwanafunzi huyo akiwa nyumbani kwake Lukumbule.

No comments: