Wednesday, November 28, 2012

TUNDURU WAITAKA SERIKALI KUWABANA VIONGOZI WASIOWAJIBIKA IPASAVYO


Na Steven Augustino,
Tunduru.

BAADHI ya wakulima wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, wameitaka serikali kuwabana viongozi wenye tabia ya kujinufaisha matumbo yao kupitia pembejeo za ruzuku ili wananchi waweze kuboresha mashamba yao katika msimu huu wa kilimo.

Hayo yalisemwa na wadau mbalimbali waliohudhuria katika mdahalo wa kukusanya maoni kupitia mdahalo wa kuwajengea uwezo juu ya utekelezaji wa shughuli za sekta ya kilimo uliowahusisha wadau wa kilimo kutoka jimbo la Tunduru Kaskazini uliofanyika ukumbi wa Skyway mjini hapa.

Kadhalika wakulima hao   walishauri kwamba serikali iangalie uwezekano wa kuondoa utaratibu wa kupeleka pembejeo hizo kwa wakulima wake na badala yake  ihamasishe wawekezaji kujenga viwanda vingi ili kuongeza uzalishaji na fedha hizo kuingizwa kama hisa katika viwanda hivyo ili mbolea au mbegu ziuzwe kwa bei nafuu.

Wakifafanua wakati wa kuchangia maoni yao kwa nyakati tofauti Bw. Sekula Matumla, Bw. Addo Makanya, Rashid Issaya, Halifa Chitemwe na Bi. Sarra Mwingira walisema kuwa hali hiyo inatokana na viongozi wa halmashauri ya wilaya hiyo wakiwemo wawakilishi wao madiwani na wabunge, kutokuwa na mwamko wa kusimamia kikamilifu ugawaji wa pembejeo za ruzuku zinazotolewa na serikali.



Walibainisha kuwa kwavile kikwazo  cha maendeleo katika wilaya ya Tunduru kinatokana na ubovu wa miundombinu ya barabara zao wakatumia nafasi hiyo kuiomba serikali kuangalia uwezekano wa kukatisha mkataba na kuifukuza Kampuni ya Progressive Higleig JV Contractors,  iliyopewa mkataba wa kujenga barabara kwa kiwango cha lami kilometa 189 kutoka wilayani Namtumbo hadi Tunduru mkoani humo, ambao ujenzi wake unasuasua hadi sasa.

Bw. John Luanda, Musa Komba na Athman Idd Milanzi walisema kuwa kitendo cha viongozi hao kushindwa kuwajibika kwa wananchi ndiko kunako sababisha vijana kuwa tegemezi kwa wazazi wao na kuwa na ulemavu wa kufikia hatua ya  kuzaa na kuacha watoto wao kwa bibi au babu zao kwa ajili ya  kulelewa wakati wao wakiwa wanatumia mtindo wa Nungunungu ambaye huchimba udongo na kuurudisha nyuma.

Wakati hayo yakiendelea pia wakulima hao wakatumia nafasi hiyo kuishauri serikali kuandaa utaratibu wa kuwakagua viongozi, ambao wamekuwa wakijinufaisha kupitia mwamvuli wa vyama vya ushirika na kubuni mbinu za makusudi kuhakikisha kuwa mikakati yake inafanikiwa.

Wachangiaji wengine ni pamoja na mwanafunzi wa shule ya sekondari Mataka; Asha Mussa, Bi. Kassiana Magogwa, Bw. Mussa Ndeka na Mussa Komba, Bi. Atingala Mohamed nao katika maoni yao waliishauri serikali kuufuta mfumo wa stakabadhi ghalani kwa madai kuwa mfumo huo, unawafanya wakulima kulipwa malipo yao zaidi ya mara moja hauna manufaa kabisa kwa zaidi ya kuwagandamiza huku wakilia na utekelezaji mbovu unaofanywa na watendaji husika.

Wakulima waliendelea kudai kuwa kitendo cha serikali kuendelea kupunguza idadi ya  pembejeo zinazopelekwa kwa wanufaika yaani  wakulima  ni swan a kurudisha nyuma maendeleo katika sekta ya kilimo.

Akizungumzia maudhui ya  mdahalo huo Mwenyekiti wa mtandao wa asasi za kiraia wilayani Tunduru(MATU) Bw. John Nginga alisema kuwa pamoja na kukusanya maoni yatakayosaidia kuboresha huduma za kilimo, alikemea pia tabia  za wananchi kutohudhuria katika mafunzo  kwa kikwazo cha vikao visivyokuwa na posho.

Akifunga madahalo huo Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Tunduru diwani Faridu Khamisi, pamoja na kuwapongeza  wafadhili wa mdahalo huo ambao ulifadhiliwa na  “The Foundation for Civil Society” aliwataka maafisa ugani kuzitumia changamoto hizo kuboresha huduma zao kwa wakulima na kutunza takwimu zitakazo wasaidia kukwepa vikwazo vya maendeleo.
 

No comments: