Saturday, November 3, 2012

UJENZI WA JENGO LA KUHIFADHIA MAITI MBINGA MASWALI MENGI KULIKO MAJIBU




Hili ni jengo la kisasa la kuhifadhia maiti katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Ujenzi wake bado unaendelea na sasa limefikia hatua ya mwisho katika kumaliza ujenzi huo. (Picha na Kassian Nyandindi)







 
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
SERIKALI nchini kupitia wizara yake ya afya imejenga jengo la kisasa la kuhifadhia maiti katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, ikiwa ni lengo la kuondokana na adha ya muda mrefu, iliyokuwa ikiikabili hospitali hiyo sehemu maalum ya kuhifadhi maiti ili zisiweze kuharibika.
   
Taarifa za uhakika zinasema kwamba ujenzi huo utagharimu shilingi milioni 145 ambapo hivi sasa kazi ya ujenzi imefikia hatua za mwisho kukamilisha jengo hilo.
   
Mradi huo unajengwa kwa kufuata michoro maalum iliyoelekezwa na wizara ya afya kupitia wataalamu wake.


Licha ya ujenzi wake kugharimu muda wa miezi minne, mpaka sasa tokea lianze kujengwa mapema mwanzoni mwa mwaka huu, muda huo umepita na bado halijakabidhiwa rasmi jambo ambalo linazua maswali mengi miongoni mwa jamii.
 
Hospitali hiyo ina zaidi ya miaka 25 mpaka sasa tokea ianzishwe haikuwa na jengo la kisasa la kuhifadhia maiti, badala yake maiti zilikuwa zikihifadhiwa kienyeji kutokana na kukosa vyombo maalum vya kuhifadhia.
 
Kadhalika jengo hilo la kuhifadhia maiti ambalo linajengwa katika hospitali ya wilaya ya Mbinga, litakuwa na uwezo wa kuhifadhi maiti 84 kwa siku katika mafriji ya kisasa yatakayohifadhiwa hapo.
 
“Mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa jengo hili mtaalamu husika ataweka mafriji ya kisasa ndani ya jengo, ambayo yataweza kutunza na kuhifadhi maiti zisiharibike”, kilisema chanzo chetu ambacho kiliomba jina lake lisitajwe.
 


No comments: